Friday, June 2, 2017

Wachezaji Yanga Kujazwa Mamilioni

Katibu mkuu wa klabu ya Yanga, Charles Boniface Mkwasa ameahidi kuwalipa wachezaji wake mishahara yao ya miezi minne wanayodai kabla ya kuanza kwa michuano ya Sportspesa Super Cup.


Kauli hiyo inakuja baada ya kuwepo kwa taarifa za wachezaji wa Yanga kutaka kususia michuano hiyo inayotarajiwa kuanza kutimua vumbi jumatatu Juni 5/17.

Mkwasa amesema kamati ya utendaji ya timu hiyo ipo katika hatua za mwisho kukamilisha malipo ya mishahara ya miezi minne ambayo wachezaji pamoja na wafanyakazi wa timu hiyo hawajalipwa hadi hivi sasa.

“Ni kweli kumekuwa na malalamiko ya hapa na pale, lakini kabla ya kuanza michuano ya Super Cup kila kitu kitakuwa kimemalizika,” alisema Mkwasa.

“Mwalimu amekabidhi ripoti yake juzi, kipindi hiki tunaipitia na baadaye tutaanza makeke yetu ya usajili,” alisema Mkwasa.

Hadi hivi sasa wachezaji ambao wamemaliza mikataba yao katika kikosi hicho cha Yanga ni Vicent Bossou, Mwinyi Haji, Donald Ngoma, Deus Kaseke, Thaban Kamusoko, Haruna Niyonzima pamoja na Amisi Tambwe.

0 comments:

Post a Comment