Sunday, July 24, 2016

ALLEGRI AKIRI KUWEPO MAZUNGUMZO NA MAN UNITED KUHUSU POGBA

Meneja wa Juventus Massimiliano Allegri amethibitisha kuwepo kwa mazungumzo kuhusu uhamisho wa Paul Pogba kwenda Manchester United kuwa bado yanaendelea.

Kuelekea kwenye mechi yao dhidi ya Atletico Madrid kwenye mashindao ya ICC (International Champions Cup), kocha huyo wa mabingwa wa Seria A aliulizwa kuhusiana na uvumi wa Paul Pogba kutimkia Old Trafford nae kuthibitisha suala hilo kwa kusema kuwa bado mazungumzo yanaendelea.
Allegri aliiambia Daily Mail kuwa Pogba ni mchezaji bado wa Juventus na wanachokifanya sasa ni kujaribu kutafuta muafaka wa mchezaji huyo.

"Pogba ni mchezaji wa Juventus kwa sasa lakini hatuna hakika na kipi kitakuja kutokea hapo mbeleni. Klabu kwa sasa ipo katika kutafuta muafaka wa suala hilo." alisema Allegri.

Hata hivyo Allegri hakuweka wazi kama ni kweli mchezaji huyo ataweka rekodi ya usajili barani ulaya kama ambavyo ripoti za vyombo mbalimbali za habari zimekuwa zikiripoti kuwa Mfaransa huyo anatarajiwa kuvunja rekodi ya usajili barani humo.

Alipoulizwa kuhusu suala hilo Jose Mourinho ambaye kwa sasa yupo ziarani na kikosi chake huko Shanghai aligoma kuzungumza chochote huku akisema kuwa yeye hawezi kumzungumzia mchezaji wa klabu nyingine.

"Sizungumzii wachezaji wa klabu zingine. Yeye (Pogba) ni mchezaji wa Juventus. Kama klabu yoyote inamhitaji mmoja wa wachezaji wangu halafu mimi nazungumzia habari za mchezaji wa klabu nyingine hiyo mimi hainifurahishi. Kwa hiyo Paul Pogba ni mchezaji wa Juventus na kitu tunachojaribu kufanya tunafanya kwa umakini, uaminifu na katika njia iliyo sahihi." alisema Mourinho.

"Kitu pekee ninachoweza kuwaambieni ni kwamba tumekamilisha asilimia 75 ya usajili wetu msimu huu, tulikuwa na mipango ya kuwanasa wachezaji wanne wa kiwango cha juu sio kwa sura bali uwezo wao na tumewapata watatu kati ya hao katika hatua za mwanzo kabisa za usajili" alimalizia Mreno huyo aliyechukua mikoba ya Louis Van Gaal katika dimba la Old Trafford.

Mashabiki wa Manchester United wamekaa kwa hamu wakisubiri kutajwa kwa jina la Paul Pogba katika kikosi huku kila kukicha habari mpya zikiendelea kuenea kuhusiana na uhamisho huo.
Ungana Na Soka24 Facebook, Bonyeza  HAPA 

0 comments:

Post a Comment