Friday, June 10, 2016

MTIBWA HAITAMBUI USAJILI WA ANDREW VICENT YANGA

Klabu ya Yanga hivi karibuni ilitangaza kumnasa mchezaji wa Mtibwa Sugar Andrew Vicent "Dante" lakini Msemaji wa Klabu ya Mtibwa, Thobias Kifaru amesema hana taarifa hizo.


Klabu ya Mtibwa Sugar imesema haijapata taarifa juu ya usajili wa  mchezaji wao Andrew Vicent 'Dante' aliyesajiliwa na Yanga hivi karibuni.

Yanga imetangaza kunasa saini za wachezaji wanne ambao ni Juma Mahadhi, Ben Kakolanya, Hassan Kessy pamoja na Andrew Vicent "Dante".

Msemaji wa klabu hiyo Thobias Kifaru amesema yeye anasikia tu tetesi kuwa mchezaji huyo amesaini Yanga, lakini hajapata taarifa rasmi kutoka kwa Mkurugenzi wake Jamal Bayser kama habari hizo ni za uhakika.

"Bado sijapata taarifa rasmi za mchezaji huyo, lakini nimesikia tu tetesi kwamba Yanga wamemchukua, labda Mkurugenzi wangu atakuwa anajua, mimi bado sijapewa taarifa zenye uhakika" alisema Kifaru.

Msemaji huyo wa klabu ya Mtibwa amesema suala zima la usajili wa wachezaji litafahamika baada ya kupata ripoti kamili ya kocha wao Mecky Maxime ndani ya wiki hii.

0 comments:

Post a Comment