Sunday, June 12, 2016

USAJILI SIMBA NI TISHIO

Mwenyekiti wa kamati ya usajili ya klabu ya Simba, Zacharia Hans Pope ametamba kuwa wamejipanga kufanya usajili wa kisayansi zaidi lengo likiwa ni kupata kikosi imara kitakachowapa ubingwa msimu ujao.

Kwa miaka mitatu mfululizo Simba hawajabeba ubingwa wa ligi kuu sababu ikisemwa kuwa ni usajili mbovu. Hans Pope amekiri kuwa wamejifunza mambo mengi katika kipindi hiki ambacho timu ilikuwa haifanyi vizuri na sasa wapo tayari kufanya mambo makubwa kutokana na usajili wao watakaoufanya. Hans Pope aliweka kambi nchini Zimbabwe akisaka wachezaji watakaoleta raha kwa mashabiki wa Simba msimu ujao.

"Simba tumepita katika wakati mgumu ukiwemo kutukanwa na kudhalilishwa kutokana na mwenendo mbaya wa timu, ukweli tumekubaliana msimu uliopita uwe mwisho na msimu ujao uwe wa vitendo" alisema Hans Pope.

"Ndio maana hivi sasa tutapambana huku na kule kutafuta kocha na wachezaji ambao watairudisha timu kama ilivyokuwa siku za nyuma." aliongeza Hans Pope ambaye aliwahi kuzingirwa na mashabiki wa Simba wakimtaka atoke katika klabu hiyo kutokana na matokeo mabaya waliyokuwa wanayapata msimu uliopita.

Hans Pope alisema Hamisi Kiiza alianza vizuri katika klabu hiyo, lakini baada ya kusifiwa alianza kuringa na kuiweka timu katika wakati mgumu na hiyo ilitokana na kukosa mtu sahihi wa kucheza nafasi yake.

0 comments:

Post a Comment