Tuesday, July 19, 2016

JOSEPH OMOG AMPA USHAURI WA BURE PLUIJM

Kocha mkuu mpya wa klabu ya Simba, Joseph Omog ametoa ushauri kwa klabu ya Yanga akiwaambia kuwa kama wanataka kufanya vizuri kwenye michuano ya shirikisho Afrika ni lazima wahakikishe wanazitumia nafasi za magoli wanazozipata.

Licha ya upinzani mkali uliopo baina ya mashabiki wa timu hizi mbili (Simba & Yanga), kocha mkuu wa Simba ameweka tofauti ya klabu hizo chini na kuamua kutoa ushauri huo kitendo kinachoashiria kuwa anapenda kuona mafanikio ya watani wake.

Yanga hadi hivi sasa imeshacheza mechi tatu, huku ikiruhusu kufungwa mbili, moja dhidi ya Mo Bejaia na nyingine dhidi ya TP Mazembe na kutoa sare moja dhidi ya Medeama na kubaki katika nafasi ya mwisho katika msimamo wa kundi A ambalo linaongozwa na TP Mazembe na kufuatiwa na MO Bejaia.

Omog ambaye amewahi kutwaa taji la michuano hiyo miaka ya nyuma akiwa na AC Leopard ya DRC Congo, anajua vizuri mbinu za kuzitumia ili kubeba taji hilo linaloshikilia nafasi ya pili kwa ukubwa baada ya lile la klabu bingwa Afrika.

"Nimekuwa nikifuatilia kwa karibu mechi zao wana timu nzuri lakini kinachowasumbua ni kukosa uzoefu kwa baadhi ya wachezaji wao na kingine ni kushindwa kuzitumia nafasi za kufunga wanazozipata kwa sababu wanatengeneza nafasi nyingi na michuano hiyo kupata nafasi siyo jambo dogo" alisema Omog.

Aidha Kocha Omog aliongeza kuwa, kufuatia kufanya vibaya katika michezo mitatu ambayo Yanga imekwishacheza tayari, cha msingi kocha Pluijm anatakiwa kuweka mkazo zaidi katika safu ya ushambuliaji na kuhakikisha wanazitumia ipasavyo nafasi wanazozitengeneza.

Tofauti na ilivyo kwa wengi hivi sasa ambao wanaona Yanga kuwa na nafasi ndogo ya kufanya vizuri na kusonga mbele katika michuano hiyo, kocha Omog yeye anawapa Yanga nafasi kubwa ya Kufanya vizuri kwenye michuano hiyo kwa kuwa watakuwa wamepata uzoefu wa kutosha katika hatua waliyofikia mwaka huu kwa kucheza na timu kubwa barani Afrika.
Ungana Na Soka24 Facebook, Bonyeza  HAPA  Kwa Habari Za Haraka Za Soka Kote Ulimwenguni.

0 comments:

Post a Comment